

Lugha Nyingine
Katibu Mkuu wa NATO aitaka Uturuki kukamilisha mchakato wa kuidhinisha Finland na Sweden kujiunga na NATO (2)
ISTANBUL - Sweden na Finland zimetimiza wajibu wao kwa Uturuki na zinapaswa kuruhusiwa kujiunga rasmi kwenye Jumuiya ya Kujihami ya Nchi za Magharibi (NATO), Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg amesema Alhamisi.
"Ni wakati wa kukaribisha Finland na Sweden kuwa wanachama kamili wa NATO," Stoltenberg amesema kwenye mkutano na waandishi wa habari huko Istanbul na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu.
"Kujiunga kwao kutafanya muungano wetu kuwa na nguvu na watu wetu kuwa salama," ameongeza, huku akibainisha kuwa Finland na Sweden ziko tayari kushirikiana kwa karibu na Uturuki kupambana na ugaidi.
Uturuki pamoja na Hungary, bado hazijakamilisha mchakato wa kuidhinisha uanachama wa NATO kwa nchi hizo mbili za Nordic licha ya kutia saini itifaki ya awali mwezi Julai.
Uturuki imekuwa ikisema mara kwa mara kwamba kabla ya mchakato huo kukamilika, Finland na Sweden lazima zichukue "hatua madhubuti" ili kupunguza wasiwasi wa Uturuki, ikiwa ni pamoja na kutia saini itifaki za kukabidhiana wahalifu na kuondoa vikwazo dhidi ya sekta ya ulinzi ya Uturuki.
Stoltenberg analenga kuharakisha mchakato wa uidhinishaji na Uturuki kwenye ziara yake ya siku tatu, ambapo pia atafanya mazungumzo na Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan na Waziri wa Ulinzi Hulusi Akar.
Hata hivyo, akijibu kauli ya Stoltenberg, Cavusoglu amesema kuwa nchi hizo mbili za Nordic hazijatimiza wajibu wao wote na zinapaswa kuchukua hatua zaidi.
"Baadhi ya hatua zilichukuliwa kwa hakika," Cavusoglu amesema. "Lakini haiwezekani kusema kwamba zimetekelezwa kikamilifu na nchi hizi mbili."
"Si nia yetu kwa kuzuia upanuzi wa (NATO)," Cavusoglu amesema. "Tunataka tu kuona hatua madhubuti."
people.cn © Tovuti ya Gazeti la Umma